Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Malawi ni kinara wa mapitio ya upunguzaji wa hatari za majanga Afrika:UNISDR

Malawi ni kinara wa mapitio ya upunguzaji wa hatari za majanga Afrika:UNISDR

Afrika imefungua ukurasa mpya katika harakati zake za utekelezaji wa mkataba wa Sendai kwa ajili ya kupunguza hatari ya majanga. Kinara ni Malawi, ambayo imefanyia tathimini na kuzipitia sera na hatua zake takribani mwaka mmoja baada ya kukumbwa na mafuriko makubwa.

Tathimini ya siku kumi nchini Malawi iliyofanywa na wataalamu watatu kutoka Msumbiji, Afrika Kusini na Zimbabwe mwezi Disemba imezindua mchakato ambao utakamilisha katika miezi ijayo uwasilishaji wa ripoti ya kwanza kabisa barani Afrika ya mapitio rika kuhusu upunguzaji wa hatari ya majanga.

Kwa mujibu wa kitengo cha Umoja wa Mataifa cha upunguzaji wa hatari ya majanga UNISDR mapendekezo yaliyotokana na mapitio rika yatakuwa muhimu katika kufanikisha na kuzuia kwa janga lingine kama la mafuriko ya 2015 nchini Malawi.

Januari 2015 watu 300 walipoteza maisha kutokana na mafuriko nchini humo huku wengine 230,000 wakikosa makazi na huduma kama chakula, maji safi, usafi, madawa na afya vikiathirika pakubwa.