Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

MINUSCA kuanzisha polisi ya kupambana na unyanyasaji wa kingono

MINUSCA kuanzisha polisi ya kupambana na unyanyasaji wa kingono

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu na Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, MINUSCA, Parfait Onanga-Anyanga ametangaza leo kuwa ujumbe huo utafungua kikosi cha polisi wa kukabiliana na wanaotekeleza unyanyasaji wa kingono na kuwalinda wanaoripoti visa vya unyanyasaji kama huo.

Katika habari zilizotolewa kwenye mtandao wa Twitter wa ujumbe huo, Mkuu huyo wa MINUSCA amesifu kujitoa kwa walinda amani katika kutenda kazi yao, lakini akawahimiza wapatie kipaumbele ulinzi wa raia na kulinda sifa ya Umoja wa Mataifa.

Bwana Onanga-Anyanga Amewakumbusha kuwa kofia zao za buluu wanazovaa zinawakilisha matumaini kwa watu walio hatarini.

Aidha, ametanganza kuwa ushirikiano unaendelea kati ya MINUSCA na Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu ili kuimarisha uwezo wa ujumbe huo wa kupambana na janga la unyanyasaji wa kingono.