Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama lalaani mashambulizi dhidi ya ubalozi wa Saudia

Baraza la Usalama lalaani mashambulizi dhidi ya ubalozi wa Saudia

Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wamelaani vikali mashambulizi ya hivi karibuni dhidi ya balozi za Ufalme wa Saudia huko Tehran na Mashhad nchini Iran yaliyosababisha uharibifu ndani ya majengo hayo. Taarifa zaidi na Joshua Mmali.

(Taarifa ya Joshua)

Kwenye taarifa yao wajumbe wamekumbusha kanuni za msingi kuhusu kuheshimu majengo ya ubalozi, na wajibu wa serikali katika kuchukua hatua ili kuzuia majengo hayo kuvamiwa au kuharibiwa.

Wanachama wameziomba mamlaka za Iran kulinda mali za ubalozi na kuheshimu wajibu wao wa kimataifa kuhusu hayo huku wakitaka pande zote kuendelea na mazungumzo na kuchukua hatua ili kupunguza mivutano kwenye ukanda huo.

Wakati huo huo mwakilishi wa kudumu wa ufalme wa Saudia kwenye Umoja wa Mataifa Balozi  Abdullah bin Yahya Almoalimi amezungumza na waandishi wa habari jijini New York na kusema.

(Sauti ya Balozi Amoalimi)

“Mashambulizi hayo hayakuwa yamechochewa na kitendo chochote cha kukasirisha. Ni ukiukwaji mkuwba wa maadili ya kimataifa, sheria na kanuni na bila shaka ni ukiukwaji mkubwa wa mkataba wa Vienna wa kulinda ofisi za ubalozi na balozi ndogo.”

Mapema katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon alieleza kusikitishwa na uvamizi na uharibifu wa majengo hayo.