Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu wenye asili ya Afrika lazima wawe na sauti katika juhudi za kukabili mkabadiliko ya tabianchi:UM

Watu wenye asili ya Afrika lazima wawe na sauti katika juhudi za kukabili mkabadiliko ya tabianchi:UM

Juhudi za kimataifa za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi lazima ziwe jumuishi zaidi kwa kushirikisha kwa kiasi kikubwa wale waliopuuzwa wakati wa mkutano wa mabadiliko ya tabianchi ya COP21. Hayo ni kwa mujibu wa taarifa ya kundi la wataalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watu wenye asili ya Afrika.

Wamesema utekelezaji wa makubaliano ya mkutano wa Paris na mazungumzo ya siku za usoni ya mabadiliko ya tabianchi lazima yazingatie mahitaji na mtazamo wa wale walio katika hatari zaidi ikiwemo watu wenye asili ya Afrika na sio tuu nguvu ya masoko.

Watu wenye asili ya Afrika ni miongoni mwa wale wanaosemekana kuathirika zaidi na mabadiliko ya tabianchi lakini hawakupewa umuhimu katika wiki mbili za mazungumzo ya COP21 mjini Paris.

Wataalamu hao wameongeza kuwa licha ya vita dhidi ya ubaguzi wa rangi na ubaguzi mwingine , iwe wa moja kwa moja au la, mara nyingi watu wenye asili ya Afrika ndio masikini zaidi, na kundi linalotengwa zaidi katika jamii. Hivyo wamesema viongozi wanaweza kufanya muafaka wa COP21 kuwa wa kihistoria kwa kuhakikisha ushiriki wa wale wanaotengwa.