Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ustawi wa watu wenye ulemavu wapigiwa chepuo Burundi

Ustawi wa watu wenye ulemavu wapigiwa chepuo Burundi

Mapema mwezi huu dunia imeadhimisha siku ya kimataifa ya watu wenye ulemavu. Ujumbe wa mwaka huu katika kuenzi siku hii ni Ujumuishwaji ni muhimu, ambapo kundi hilo lililoachwa nyuma kwa muda mrefu linapigiwa chepuo na jumuiya ya Kimataifa ili lijumuishwe katika kila nyanja, ikiwamo elimu, afya, miundombinu na huduma za kijamii kwa ujumla. Kwa mantiki hiyo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon akitoa ujumbe wake wa siku hiyo amesema wakati dunia ikiadhimisha siku ya kimataifa ya walemavu, malengo ya maendeleo endelevu yaani agenda 2030 yanayotekelezwa na dunia yanapaswa kuwajumuisha watu wenye ulemavu.

Ban amenukuliwa akisema kuwa malengo hayo yanataka mtu yeyote asiachwe nyuma na hivyo akataka kundi hilo lihakikishiwe ustawi wake kwa kila nyanja. Katika kuhakikisha hilo, Shirika la kazi ulimwenguni ILO kwa kushirikiana na makampuni 11 ambayo yamekuwa wadau wa kwanza kusaini mkataba kuhusu ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu katika maeneo ya kazi wako mstari wa mbele kutetea maslahi ya kundi hilo kote duniani .

Taarifa ya ILO inasema kuwa kazi hiyo ya kimataifa iliyoko  chini ya mkataba wa mtandao wa walemavu inahusu maeneo mengi ya ulinzi dhidi ya kundi hilo ikiwamo kuwalinda dhidi ya ubaguzi. Je watu wenye uleamavu wanajumuishwa na kuwezeshwa ipasavyo katika kila ngazi? Nao wenyewe wanasemaje? Tuelekee nchini Burundi ambako maadhimisho hayo yamefanyika. Tuungane na mwandishi wetu wa maziwa makuu Ramadhani Kibuga.