Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Azimio 2254 kuhusu Syria lakaribishwa

Azimio 2254 kuhusu Syria lakaribishwa

Kamisheni huru ya uchunguzi kuhusu Syria imekaribisha kupitishwa kwa azimio namba 2254 la Baraza la Usalama kuhusu mchakato wa amani nchini Syria.

Kwenye taarifa yake iliyotolewa leo, Kamisheni hiyo imesema azimio hilo ni hatua muhimu ya kwanza kuelekea amani ya kudumu nchini humo.

Aidha imeelezea kwamba azimio la Baraza la Usalama lililopitishwa tarehe 17 Disemba kuhusu ufadhili wa ugaidi litasaidia kupambana na waasi wa ISIL ambao ni tishio kubwa kwa amani ya kimataifa.

Hatimaye Kamisheni hiyo imesisitiza umuhimu wa kulinda usalama wa raia na haki za binadamu hata wakati wa kupambana na ISIL.

Azimio 2254 la Baraza la Usalama limeuomba Umoja wa Mataifa kuhamasisha utaratibu wa kisiasa utakayoongozwa na wasyria wenyewe ili kuanzisha serikali mpya na jumuishi itakayoaminika na wasyria wote.