Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haki za usafi wa mazingira na maji ni haki za binadamu:UM

Haki za usafi wa mazingira na maji ni haki za binadamu:UM

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki yya binadamu ya maji na usafi wa mazingira Léo Heller, na mwenyekiti wa tume ya Umoja wa mataifa ya uchumi, jamii na haki za kitamaduni Waleed Sadi, leo wamekaribisha kutambuliwa na baraza kuu la Umoja wa mataifa kwa haki ya binadamu ya usafi wa mazingira kuwa kama haki ya msingi pamoja na haki ya binadamu ya maji salama ya kunywa .

Zaidi ya watu bilioni 2.5 bado hawana fursa ya mazingira safi, huku lengo la usafi lililo ndani ya lengo nambari 7 la maendeleo ya milenia limeshindwa kufikiwa kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na vipenge vingine 18 vya malengo ya maendeleo ya milenia.

Watu bilioni moja bado wanajisaidia kwenye maeneo ya wazi, watu tisa kati ya kumi hasa katika maeneo ya vijijini. Bwana Sadi amesema haki ya usafi wa mazingira ni kipengee muhimu cha haki ya kuwa na maisha bora inayoingiliana na kuwa na afya njema, na haki ya binadamu ya maji.

Naye Bwana Heller amesema usafi wa mazingira na masuala ya maji yanahitaji kupewa uzito wa juu katika ngazi zote, na maana ya haki ya binadamu ya usafi wa mazingira na haki ya binadamu ya maji zilizobainishwa kwenye azimio la baraza kuu zitasaidia mtazamo wa kimataifa kufikia malengo ya masuala ya usafi kwa ajenda ya 2030 ya maendeleo.