Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Msiwanyanyase watetezi wa haki za binadamu Palestina:UM

Msiwanyanyase watetezi wa haki za binadamu Palestina:UM

Wataalamu huru wa Umoja wa mataifa leo wameelezea hofu yao kufuatia ripoti zinazoendelea kwamba watetezi wa haki za binadamu wamekuwa wakikabiliwa na mashambulizi, unyanyasaji, kukamatwa na kuwekwa kizuizini pamoja na vitisho vya kuuawa hususani kwenye eneo la Hebron kwenye eneo linalokaliwa la mamlaka ya Wapalestina. Hii ni hatua za uongozi wa Israel na walowezi kutaka kuzuia kazi zao muhimu na za amani.

Kwa mujibu wa Michel Forst mwakilishi maalumu wa Umoja wa mataifa kuhusu hali ya watetezi wa haki za binadamu, wakati ghasia zimechacha katika miezi kadhaa iliyopita kwenye eneo linalokaliwa la Wapalestina, Wapalestina na watetezi wa haki za binadamu wamekuwa wakitoa ulinzi kwa wale waliko katika hatari ya ghasia na kuorodhesha ukiukwaji wa haki za binadamu.

Kuendelea kunyanyaswa kwa watetezi hao wa haki za binadamu ambao wanatekeleza uhuru wao wa kujieleza ni jambo lisilokubalika na ni lazima likomeshwe mara mora amesema bwana Forst.

Kauli ya wataalam hao imepitishwa na mwakilishi maalumu kuhusu mateso na ukatili mwingine, unyama au udhalilishaji au adhabu, bwana, Juan E. Méndez, na mwakilishi maalumu juu ya haki ya uhuru wa kukusanyika kwa amani bwana Maina Kiai.