Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Historia kuandikwa katika uchaguzi ujao wa Katibu Mkuu wa UM:

Historia kuandikwa katika uchaguzi ujao wa Katibu Mkuu wa UM:

Nchi wanachama wa Umoja wa mataifa kwa mara ya kwanza watajumuishwa kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi wa Katibu Mkuu ajaye wa Umoja wa mataifa, amesema Rais wa baraza kuu la Umoja wa mataifa hii leo.

Mchakato wa uchaguzi wa mkuu huyo wa Umoja wa mataifa umeanza rasmi Jumanne kufuatia kupelekwa kwa barua maalumu kwa nchi zote wanachama 193 wa Umoja wa mataifa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa mataifa anateuliwa na baraza kuu kutokana na mapendeklezo ya baraza la usalama. Awe mwanamke au mwanaume , atakayeteuliwa atamrithi Ban Ki-moon ambaye muhula wake wa miaka 10 utakamilika miezi 12 ijayo.

Barua hiyo imetolewa kwa pamoja na rais wa baraza la usalama na Rais wa baraza kuu Mogens Lykketoft, ikielezea umuhimu wa wa uwazi na ujumuishi katika mchakato wa uchaguzi huo ambao utajumuisha majadiliano na nchi wanachama, jambo ambalo ni hatua kubwa mpya.

Huyu hapa Mogens Lykketoft..

(SAUTI YA MOGENS LYKETOFT)

"Mchakato huu umeanza na matumaini kwamba wanachama kwa mara ya kwanza katika historia ya Umoja wa mataifa wajumuishwe kikamilifu katika majadiliano yahusuyo katibu mkuu ajaye."

Inatarajiwa kwamba majina ya wagombea yatawasilishwa mwishoni mwa mwezi Machi mwakani na Katibu Mkuu mpya ataanza majukumu yake Januari 2017 kwa awamu ya miaka mitano ambayo inaweza kuongezwa nan chi wanachama kwa miaka mitano Zaidi.