Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wadau wa mzozo wa Yemen kuanza mazungumzo Disemba 15

Wadau wa mzozo wa Yemen kuanza mazungumzo Disemba 15

Huko Mashariki ya Kati, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Yemen, Ismail Ould Cheikh Ahmed ameitisha mkutano tarehe 15 Disemba nchini Uswisi ambapo atakuwa na mazungumzo na wadau wa Yemen kwa ajili ya kuafikia sitisho la mapigano na kuimarisha hali ya kibinadamu nchini humo.

Akiongea na waandishi wa habari mjini Geneva, Bwana Ahmed amesema lengo la mazungumzo hayo ni kurejea utaratibu wa mpito wa kisiasa, ambao amesema ni suluhu ya pekee kwa mzozo wa Yemen, kupitia mazungumzo jumuishi.

Serikali ya Yemen na wahouthi wameshakubali kushiriki mazungumzo hayo yatakayoongozwa na Mjumbe huyo maalum, ambaye amewataka wadau wote kuchuka hatua stahiki.

(SAUTI OULD)

‘‘Nazitaka pande zote kuzingatia usitishwaji wa mapigano hima mnamo Desemba 15, ili kuandaa mazingira bora ya majadiliano ya amani, kuokoa maisha, na kutoa tumaini kwa watu wa Yemen.’’