Ban amteua Michael Keating kumrithi Kay Somalia
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amemteua Michael Keating wa Uingereza kuwa mwakilishi wake maalum nchini Somalia na mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNSOM .
Keating anachukua nafasi ya Nicholas Kay wa Uingereza pia ambaye anamaliza muda wake mwisho wa mwaka huu.
Taarifa ya msemaji wa Katibu Mkuu inasema kuwa Ban amemshukuru Kay kwa uongozi wake thabiti kwa UNSOM kwa miaka miwili na nusu ikiwa ni kipindi muhimu kwa mpito wa kisiasa kwa Somalia.
Taarifa hiyo inasema kuwa mteule huyo Bwana Keating ana uzoefu katika masuala ya kisiasa na ujenzi wa amani pamoja na masuala ya kibinadamu. Amewahi kushika wadhifa wa mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu na mratibu wa masuala ya kibinadamu nchini Afghanistan kuanzia mwaka 2010 hadi 2012.