Ubaguzi wa kitaifa kwa misingi ya uzawa ushughulikiwe: Zeid
Kamati ya Baraza la haki za binadamu kuhusu utokomezaji wa ubaguzi wa rangi imeanza kikao chake cha 88 huko Geneva, Uswisi ambapo Kamishna Mkuu wa haki za binadamu kwenye Umoja wa Mataifa Zeid Ra’ad Al Hussein, amepazia sauti suala la uzawa ambalo linaonekana kuchochea ubaguzi kwa misingi mbalimbali.
Katika hotuba yake Kamishna Zeid amesema kuwa dhana ya uzawa yenye misingi ya kibaguzi ni hatari kwani inaweza kuleta matabaka miongoni mwa jamii husika.
(SAUTI ZEID)
‘‘Tunachokiona kinaibuka katika sehemu nyingi duniani ni suala la utaifa kwa misingi ya uzawa, likijinasibu kwa hali ya hatari sana na mara nyingi tunaona serikali zikipindisha mambo na kupandikiza chuki dhidi ya makundi kwa misingi ya kabila na rangi . Kazi ya kamati hii ni muhimu katika kushughulikia suala hili. ‘’
Amesema kuwa katika kukabiliana na dhana ya uzawa na athari zake katika jamii bado mambo mengi hayajafanywa kutokana na changamoto ambazo dunia imekumbana nazo.