Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mratibu wa kibinadamu Libya akaribisha kuachiliwa kwa waliotekwa

Mratibu wa kibinadamu Libya akaribisha kuachiliwa kwa waliotekwa

Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu nchini Libya, Ali Al-Za’tari, amekaribisha kuachiliwa kwa wahudumu wawili wa kibinadamu baada ya miezi mitano matekani, na kuwashukuru wote waliosaidia katika kuhakikisha raia hao wa Libya wanaachiliwa.

Mohamed al-Monsef Ali al-Sha’lali na Walid Ramadan Salhub walikuwa wanapeleka misaada kusini magharibi mwa Libya walipokamatwa mnamo Juni 5, 2015 huko al-Shwayrif, kusini mwa nchi.

Wanaume hao waliokuwa wanafanya kazi na shirika la kibinadamu la Shaik Tahir Azzawy – ambalo husaidia mashirika kadhaa ya kimataifa katika kutekeleza shughuli zao – waliachiliwa huru mnamo Novemba 7, 2015.Akieleza kufurahishwa na kurejea kwao wakiwa salama kwa familia zao, Bwana Ali Al-Za’tari, amesisitiza haja ya kuwezesha usambazaji wa misaada ya kibinadamu kwa njia salama kote nchini, akiongeza kwamba kuwafikishia misaada wenye uhitaji kunapaswa kulindwa na kutoathiriwa na migogoro.