Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM Burundi yaokoa familia zilizoathirika na mafuriko

IOM Burundi yaokoa familia zilizoathirika na mafuriko

Nchini Burundi, Shirika la Kimataifa la Uhamiaji IOM limeanzisha mradi wa kuzipatia makazi ya muda familia 375 zilizopoteza nyumba zao kwa sababu ya mafuriko. Taarifa zaidi na Assumpta Massoi

(Taarifa ya Assumpta)

Kwa mujibu wa IOM, zaidi ya watu 65,000 wako hatarini kuathirika na mafuriko nchini humo kwenye mikoa kumi na moja kutokana na mvua kali zilizosababishwa na El-nino.

Akizungumza na idhaa hii leo, Aloys Ngaruko, msaidizi wa miradi wa IOM, tayari wameshajenga mahema 140 kwa kundi la kwanza lililolengwa miongoni mwa familia zinazoishi kwenye mazingira magumu zaidi.

(Sauti ya Bwana Ngaruko)

Hata hivyo amesema vifaa vya akiba vya IOM Burundi havitatosha kusaidia watu wote walioathirika na mafuriko na ufadhili unahitajika kwa dharura ili kutimiza mahitaji yao.

Kwa ujumla ni dola milioni 16 ambazo zinahitajika kwa ajili ya kutekeleza mradi wa kuchukua hatua kwa dharura dhidi ya mafuriko unaotekelezwa kwa ushirikiano na Shirika la Kimataifa la Msalaba Mwekundu ICRC.  Kwa upande wake IOM inahitaji dola milioni 7 kwa ajili ya kutekeleza operesheni zake kwenye mpango huo.