Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban na Dkt. Zuma wajadili Burundi

Ban na Dkt. Zuma wajadili Burundi

Leo Jumanne Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amekuwa na mazungumzo ya simu na Mwenyekiti wa kamishen ya Muungano wa Afrika, AU, Dkt. Nkosazana Dlamini Zuma kuhusu hali ya usalama Burundi.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa ameeleza kuwa katika mazungumzo hayo, Ban amekaribisha uamuzi wa tarehe 17 mwezi huu wa baraza la amani na usalama la AU wa kushughulikia mkwamo wa kisiasa na kuzorota kwa hali ya usalama nchini humo.

Amesema azma ya aina hiyo inaweza kuipatia Burundi fursa ya kuweka kando ghasia zinazoendelea kila uchao na kupata maridhiano ya pamoja ya kisiasa.

Katibu Mkuu amemhakikishia Dkt. Nkosazana kuwa Umoja wa Mataifa uko tayari kutoa msaada wowote muhimu wa kusongesha utekelezaji wa hatua zitakazokubaliwa na wanachama wa baraza hilo la amani na usalama la muungano wa Afrika.