Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kilimo cha mpunga chapata mwongozo wa uendelevu na uwajibikaji kijamii

Kilimo cha mpunga chapata mwongozo wa uendelevu na uwajibikaji kijamii

Mwongozo wa kwanza wa kilimo endelevu cha mpunga, ambao unaweka viwango wastani vipya katika kilimo cha zao hilo, umezinduliwa leo na muungano wa taasisi za utafiti katika kilimo cha mpunga duniani, SRP  na Shirika la Mpango wa Mazingira, UNEP.

Mwongozo huo wa kilimo endelevu cha mpunga unatumia viwango wastani vinavyojali mazingira na jamii, ili kuendeleza uzalishaji bora wa mpunga kwa wakulima wadogowadogo, kupunguza madhara ya kilimo cha mpunga kwa mazingira na kukidhi mahitaji ya watumiaji ya uhakika na ubora wa chakula.

Utungaji wa mwingozo huo uliongozwa na SRP, Shirika la Taasisi ya Kimataifa ya utafiti katika kilimo cha mpunga, IRRI, shirika la UTZ Certified na Shirika la Aidenvironment, ukifuata uzoefu uliotokana na mikakati mingine endelevu katika bidhaa nyingine kama miwa, pamba, kahawa na mawese.

Mwongozo unajumuisha masuala 46, yakiwemo uzalishaji, uhakika wa chakula, afya ya wafanyakazi, haki za wafanyakazi na bayo annuai.

Mpunga huchangia kwa kiasi kikubwa katika uhakika wa chakula duniani, na ni kitega uchumi cha kutegemewa kwa zaidi ya wakulima wadogowadogo milioni 140 katika nchi zinazoendelea.