Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban awasili Israel baadaye kuelekea Palestina

Ban awasili Israel baadaye kuelekea Palestina

Siku moja baada ya kutoa ujumbe wake kwa waisraeli na wapalestina, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amewasili Mashariki ya Kati kwa lengo la kukutana na viongozi wa Palestina na Israel. Taarifa zaidi na Assumpta Massoi.

(Taarifa ya Assumpta)

Ban ameanzia Israel ambapo tayari amekutana na Rais wa nchi hiyo Reuben Rivlin akitoa pole kwa wahanga wa mashambulizi. Katika mkutano na waandishi wa habari Ban amesema hakuna jamii inapaswa kuishi kwa woga na kwamba ni vema kurejelea mazungumzo.

(Sauti ya Ban)

Katibu Mkuu atakutana pia na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyau na Rais wa mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas pamoja na viongozi waandamizi. Awali katika ujumbe wake wa video kwa pande mbili hizo, Ban alitoa rai kwa wapalestina.

(Sauti ya Ban-1)

"Naelewa kukata tamaa kwenu. Najua matumaini yenu ya amani yamevunjwa mara nyingi. Na kwa viongozi wa Palestina, nasema hivi:Unganisheni nguvu za watu wenu kwa njia ya amani ili kuwawezesha kufikia ndoto matamanio yao."

Ban amesema Umoja wa Mataifa upo pamoja na pande hizo na utaendelea kuunga mkono juhudi za kuweka mazingira ya kurejelea mashauriano yenye maana na kwamba hakuna kukata tamaa.