Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Zaidi ya watu Milioni 100 wahitaji misaada ya kibinadamu duniani kote: OCHA

Zaidi ya watu Milioni 100 wahitaji misaada ya kibinadamu duniani kote: OCHA

Zaidi ya watu Milioni 100 duniani kote wanahitaji misaada ya kibinadamu ambapo Umoja wa Mataifa umesema hiyo ni idadi ya kutisha.

Kauli hiyo imetolewa na Stephen O’Brien, msaidizi wa Katibu Mkuu kuhusu masuala ya usaidizi wa kibinadamu kwenye Umoja wa Mataifa wakati akifungua mashauriano ya kimataifa kuelekea mkutano wa usaidizi wa kibinadamu mwezi mei mwakani huko Istanbul, Uturuki.

Amesema mizozo inaoongoza kwa kuchochea ongezeko la mahitaji ya kibinadamu duniani wakati huu ambapo licha ya usaidizi kutolewa bado mahitaji yanapanda.

(Sauti ya O’Brien)

"Misaada ya kibinadamu inafikia watu wengi zaidi na katika maeneo mengi zaidi duniani kuliko wakati wowote ule. Lakini bado idadi ya wahitaji inaongezeka. Mwaka hadi mwaka, kiwango cha gharama ya kukidhi mahitaji ya kibinadamu kinazidi uwezo wetu wa kuyakidhi.”

Kwa mujibu wa O'Brien ambaye pia ni mkuu wa ofisi ya usaidizi wa kibinadamu, OCHA, majanga ya kiasili nayo ni chanzo cha ongezeko la usaidizi wa kibinadamu akisema yanasababisha kila mwaka hasara ya kiuchumi ya karibu dola Bilioni 300.