Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF, WHO wakabiliana na Polio Ukraine

UNICEF, WHO wakabiliana na Polio Ukraine

Majuma sita baada ya mlipuko wa Polio nchini Ukraine mashirika ya Umoja wa Mataifa, lile la kuhudumia watoto UNICEF pamoja na la afya WHO, yameingilia kati kwa kuendesha awamu ya kwanza ya chanjo kitaifa.

Wizara ya afya ya Ukraine tayari imethibitisha visa viwili vya polio Kusini mwa nchi mnamo Septemba mosi, ambapo watoto waliogundulika wana umri wa miezi 10 na miaka minne na hawakuwahi kupata chanjo dhidi ya ugonjwa huo.

Kwa mujibu wa UNICEF viwango vya kimataifa vinaeleza kuwa kisa kimoja chaweza kusababisha mlipuko wa haraka miongoni mwa watoto ikiwa chanjo haitatolewa nakupendekeza awamu tatu za chanjo dhidi ya polio na shirika hilo limenunua vifaa milioni 3.7 vya chanjo vilivyothibitishwa ubora na WHO.

Ikiwa hautadhibitiwa haraka ugonjwa wa polio unaoshambulia watoto unaweza kuenea Ukarine na kuhatarisha maisha ya watoto milioni 1.8 imesema UNICEF.