Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama lalaani shambulizi dhidi ya MINUSCA

Baraza la Usalama lalaani shambulizi dhidi ya MINUSCA

Wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wamelaani vikali mashambulizi dhidi ya msafara wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kuweka utulivu nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, MINUSCA uliokuwa unatoka eneo la Damara hadi Ngerengou huko Ombela- Mpoko, ambapo mlinda amani mmoja kutoka Burundi aliuawa na mwingine kujeruhiwa.

Katika taarifa wanachama wa Baraza hilo pamoja na kulaani mashambulizi yote na uchokozi unaofanywa na waasi dhidi MINUSCA wamesisitiza kwamba, mashambulizi ya kulenga walinda amani wa Umoja wa Mataifa yanaweza kuwa uhalifu wa kivita na kuwakumbusha pande zote katika mgogoro nchini CAR kuhusu wajibu wao kwa mujibu wa sheria ya kimataifa ya kibinadamu.

Kwa maantiki hiyo, wanachama hao, wametoa wito kwa mamlaka ya Jamhuri ya Afrika ya Kati kufanya uchunguzi wa haraka, kwa ushirikiano na  MINUSCA,  na kuwafikisha wahusika mbele ya sheria.