Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

CITES yataka usafiri wa anga ujiunge na mapambano dhidi ya biashara haramu ya wanyamapori

CITES yataka usafiri wa anga ujiunge na mapambano dhidi ya biashara haramu ya wanyamapori

Katibu Mkuu wa Mkataba wa Biashara ya Kimataifa kuhusu viumbe walio katika hatari ya kuangamia (CITES) John E. Scanlon amesema makundi ya uhalifu ya kimataifa yanatumia njia halali za usafiri kusafirisha bidhaa zao za magendo, mathalan pembe za vifaru vinasafirishwa kupitia kwa ndege, huku pembe mbichi za ndovu zikisafirishwa kupitia kwa bahari.

Akihutubia mkutano wa kimtaifa endelevu wa Kundi la utendaji kazi kuhusu Usafiri wa Anga uliofanyika mjini Geneva, Uswisi Scanlon amesema, biashara haramu ya viumbe wa pori imekithiri, lakini katika mazingira ya wingi wa jumla wa usafiri wa anga na bahari, mara nyingi ni sehemu ndogo tu ya mizigo au maabiria wanaobeba bidhaa haramu ya wananyamapori kinyume cha sheria.

Aidha, Scanlon amesema kuna juhudi za pamoja za kimataifa zinazoendelezwa na serikali, Umoja wa Mataifa, mashirika ya kitaifa na ya kimataifa, taasisi za kihisani, sekta binafsi, jamii na watu binafsi za kupambana na biashara haramu ya wanyamapori.

Akitoa mfano, wiki iliyopita, Umoja wa Mataifa ilipitisha Ajenda ya Manedeleo Endelevu, SDG’s ambapo mojawapo ya ajenda hiyo ni kukomesha ujangili na magendo.

Katika dunia ya sasa ya utandawazi, watalii bilioni 1.1 wanasafiri kila mwaka, ndege 100,000 zinasafiri kila siku na makasha milioni 5000 yanasafirishwa kwa meli kila mwaka.