Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban awa na mazungumzo na Rais Zuma jijini New York

Ban awa na mazungumzo na Rais Zuma jijini New York

Kando mwa vikao vya malengo ya maendeleo endelevu, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amekuwa na mazungumzo na Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini ambapo amemshukuru kwa ushirikiano ambao nchi yake inapatia Umoja wa Mataifa hususan masuala ya usalama na amani.

Taarifa ya msemaji wa Umoja wa Mataifa imesema Ban na Zuma katika muktadha huo wa amani na usalama wamejadili hali ya usalama Burundi, Sudan Kusini na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo , DRC sanjari na dhima ya Afrika Kusini katika kikosi cha kujibu mashambulizi kwenye ujumbe wa Umoja wa Mataifa huko DRC, MONUSCO.

Halikadhalika Ban amekaribisha ushiriki wa Afrika Kusini katika jitihada za kimataifa za kukabili mabadiliko ya tabianchi sanjari na maendeleo endelevu.

Masuala mengine waliyojadili ni yale ya Umoja wa Mataifa ikiwemo marekebisho ya baraza la usalama.