Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban akaribisha makubaliano baina ya serikali ya Colombia na waasi wa FARC kuhusu wahanga

Ban akaribisha makubaliano baina ya serikali ya Colombia na waasi wa FARC kuhusu wahanga

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amekaribisha makubaliano yaliyofikiwa kati ya serikali ya Colombia na waasi wa FARC kuhusu masuala ya wahanga, hapo jana Septemba 23 mjini Havana, Cuba.

Ban amepongeza pande zote kwa kutoa kipaumbele kwa maslahi ya waathiriwa katika mchakato wa amani.

Taarifa ya msemaji wake imesema makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kuelekea kufikia mkataba wa amani, na kuisongesha Colombia karibu zaidi kuumaliza mzozo uliodumu miaka mingi zaidi kaskazini mwa sayari dunia.

Akiongea na Redio ya Umoja wa Mataifa Fabrizio Hochschild, Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Colombia amefuraishwa na makubaliano hayo ya kihistoria akisema iwapo yatatekelezwa yataleta mabadiliko makubwa.

« Siyo tu kwamba tutamaliza moja ya mizozo ya muda mrefu zaidi duniani, bali pia makubaliano hayo yataleta mabadiliko makubwa nchini Colombia. Yatafungua milango ya maendeleo na ukuaji wa uchumi, na kumaliza shughuli haramu za kiuchumi zinazoleta madhara kwenye eneo hilo na duniani kote. »