Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hoja ya kutaka kumshtaki Rais Somalia imalizwe kwa mashauriano:Kay

Hoja ya kutaka kumshtaki Rais Somalia imalizwe kwa mashauriano:Kay

Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Nicholas Kay amekaribisha mwenendo ambao kwao pande husika nchini humo zinajikita katika kupatia suluhu mzozo juu ya hoja ya kumfungulia mashtaka Rais wa nchi hiyo na kupongeza ari yao ya kuhakikisha kuna amani na utulivu.

Taarifa ya ofisi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, UNSOM ambayo inaoongozwa na Bwana Kay, imemnukuu akikaribisha jitihada za spika wa bunge la taifa na kamati inayohusika na hoja hii ya kufanya kazi kwa dhati kupatia suluhu suala hilo kwa njia ya mashauriano.

Amewasihi wadau wote kusongesha harakati za kupatia suluhu mzozo huo wa sasa, hatua ambayo amesema itawezesha mchakato wa kisiasa nchini Somalia kuendelea bila vikwazo.

Bwana Kay amewataka wadau hao kushirikiana katika kuzindua jukwaa la mashauriano ili kuunda mchakato wa uchaguzi wa mwaka 2016 utakaotokana na wasomali wenyewe.