Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Changamoto yetu ya pamoja ni kutimiza uwezo mkubwa zaidi wa utalii- Ban

Changamoto yetu ya pamoja ni kutimiza uwezo mkubwa zaidi wa utalii- Ban

Utalii huchangia pakubwa katika kufungua nafasi za ajira, kupunguza umaskini, kuwezesha wanawake, kutunza mazingira na kujenga amani, na changamoto ya pamoja ni kutimiza hata uwezo mkubwa zaidi wa sekta hiyo ambayo ni moja ya sekta kubwa zaidi na zinazokuwa kwa kasi zaidi. 

Huo ni ujumbe alioutoa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon kwa kikao cha 21 cha Baraza Kuu la Shirika la umoja wa Mataifa la Utalii, UNWTO, kupitia njia ya video.

Baraza hilo linakutana mjini Medellin, Colombia. Ban amesema amefurahishwa na kwamba UNWTO inahusika kikamilifu katika michakato mbalimbali ya mfumo wa Umoja wa Mataifa, hususan ile inayomulika nchi za visiwa vidogo zinazoendelea, nchi maskini na nchi zisizo na pwani.

Aidha, Katibu Mkuu amesifu mchango unaoongezeka wa UNWTO katika ajenda ya kimataifa ya usalama.

Amesema anategemea shirika hilo kuhusika kikamilifu katika kutimiza ajenda ya maendeleo endelevu, ambayo kwa mara ya kwanza kabisa, yanajumuisha malengo yanayohusiana na utalii endelevu.