Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Matumaini yapo kwa maridhiano kati ya Korea Kusini na Kaskazini: mtalaam wa UM

Matumaini yapo kwa maridhiano kati ya Korea Kusini na Kaskazini: mtalaam wa UM

Mratibu Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya watu wa Korea DPRK Marzuki Darusman amesema mawasiliano kati ya DPRK na Jamhuri ya Korea yameanza kubadilika.

Kwenye taarifa iliyotolewa leo baada ya ziara yake ya siku tano nchini Jamhuri ya Korea, Bwana Darusman amesema wawakilishi wa nchi hizo mbili wamekutana na kuzungumzia jinsi ya kuunganisha familia zilizotenganishwa tangu Korea ilipogawanywa kwenye sehemu mbili.

Ameongeza kuwa watu wanazidi kuzungumzia uwezekano wa kuungana tena kwa nchi hizo mbili.

Ziara yake ni ya kwanza baada ya kufunguliwa kwa ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za binadamu mjini Seoul, Jamhuri ya Korea kwa ajili ya kufuatilia hali ya haki za binadamu nchini DPRK.

Bwana Darusman amesisitiza kwamba ripoti ya Ofisi ya Haki za Binadamu imebaini ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu nchini DPRK na hatua zinapaswa kuchukuliwa ili kukabili na hali hiyo.