Azimio la kuendeleza usawa wa jinsia lahitaji msukumo
Haki za wanawake zinakabiliwa na hatari ya kurudi nyuma, licha ya azimio kuu la Umoja wa Mataifa lililolenga kuendeleza usawa.
Onyo hilo limetolewa kwenye kongamano la kufanyia tathmini hatua zilizopigwa kimataifa kuendeleza usawa wa jinsia, kutokana na azimio la Baraza la Usalama nambari 1325 lililopitishwa miaka 15 iliyopita, kuhusu wanawake, amani na usalama.
Wajumbe katika kongamano hilo linalofanyika mjini Geneva wameambiwa kuwa licha ya maendeleo yaliyopatikana katika miaka ya hivi karibuni, haki za msingi za wanawake bado zimetelekezwa au kukiukwa.
Bineta Diop ni mjumbe wa Muungano wa Afrika, AU, ambaye ana jukumu la kuhakikisha kuwa sauti za wanawake zinasikika katika ujenzi wa amani na utatuzi wa mizozo:
“Ukienda mashinani na kuuliza kuhusu azimio 1325, watakwambia, ‘hatujui chochote kuhusu 1325’ lakini ukiongea nao kuhusu ulinzi wa wanawake, wanaelewa. Ukiongea kuhusu haki zao, wanaelewa 1325 kwa misingi hiyo.”