Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanafunzi nusu milioni wa Palestina kutoenda shuleni iwapo ufadhili hautapatikana

Wanafunzi nusu milioni wa Palestina kutoenda shuleni iwapo ufadhili hautapatikana

Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia wakimbizi wa Palestina UNRWA limetuma ripoti ya dharura ya fedha kwa Katibu Mkuu Ban Ki-moon likisema ukosefu wa ufadhili unaweza kuchelewesha wanafunzi nusu milioni kwenda shuleni.

Taarifa iliyotolewa leo imesema iwapo mahitaji ya UNRWA ya ufadhili ya dola milioni 101 hayatatimizwa ifikapo katikati mwa mwezi wa  Agosti,UNRWA italazimika kusitisha utoaji wa baadhi ya huduma, ikiwemo kuahirisha ufunguzi wa shule 700 na shule nane za ufundi.

UNRWA imeongeza kuwa tayari ilibidi utoaji huduma upunguzwe na sasa hivi UNRWA inaendelea kutoa huduma za kuokoa maisha tu, huku uamuzi huo ukisababisha mvutano kwenye kambi 58 za UNRWA, wakimbizi na wafanyakazi wa UNRWA wakipinga uamuzi huo.

Kamishna Mkuu wa UNRWA Pierre Krahenbuhl ameeleza wasiwasi wake kuhusu hatua zilizochukuliwa na UNRWA akisema muda huu ni wakati ambapo msaada wa UNRWA bado unahitajika sana kwa wakimbizi wa Palestina.