Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM na UNHCR zatoa mafunzo kwa wadau Libya kuhusu kunusuru maisha baharini

IOM na UNHCR zatoa mafunzo kwa wadau Libya kuhusu kunusuru maisha baharini

Shirika la Kimataifa la Uhamiaji, IOM na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR, yameandaa warsha ya siku mbili mjini Tripoli ili kuwapa mafunzo wadau nchini Libya kuhusu kuyanusuru maisha ya wahamiaji kwenye pwani ya Libya.

Warsha hiyo ilifadhiliwa na idara ya usaidizi wa kibinadamu na ulinzi wa raia katika Kamisheni ya Ulaya, ECHO, na imehudhuriwa na maafisa 19 kutoka kwa walinzi wa pwani ya Libya na idara ya usalama wa bandari, idara ya kupambana na uhamiaji haramu na maafisa wawili wa Hilali Nyekundu ya Libya.

Mkutano huo ulitoa fursa ya aina yake ya kutathmini hali ya sasa na utaratibu unaohusiana na kunusuru maisha baharini, ukiwemo kuwatambua wahamiaji walio hatarini na utoaji wa usaidizi wa kibinadamu mara moja wanapowasili kwenye bandari ya Libya.