Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza Kuu lataka kutokomeza ujangili wa wanyamapori

Baraza Kuu lataka kutokomeza ujangili wa wanyamapori

Leo Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa limepitisha azimio la kuzisihi nchi wanachama kuchukua hatua thabiti ili kuzuia na kutokomeza biashara haramu ya wanyamapori, likisema wanyama hao ambao wako hatarini kutoweka hawataweza kubadilishwa.

Azimio la Baraza hilo limemulika ongezeko la ujangili wa vifaru na tembo barani Afrika, likisema biashara haramu ya wanyama pori siyo tu hatari kwa mifumo ya ekolojjia na kuwepo kwa wanyama hawa, bali pia inaathiri jamii, sekta ya utalii na hatimaye juhudi za kukuza maendeleo endelevu.

Mapendekezo ya azimio hilo ni kuimarisha mifumo ya sheria ili kuchunguza na kudhibiti vitendo vya ujangili, aidha kuboresha utekelezaji wa adhabu zinazohukumiwa.

Kadhalika azimio linaziomba nchi wanachama kushirikiana zaidi na kulinganisha mifumo yao ya sheria.