Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Muda umefika kuondoa vizuizi dhidi ya Iran na Cuba

Muda umefika kuondoa vizuizi dhidi ya Iran na Cuba

Mtalaam huru wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu na vizuizi Idriss Jazairy, amesema muda umefika kuondoa vizuizi dhidi ya Cuba na Iran ili kulinda haki za watu wanaotesekea zaidi nchini humo.

Kwenye mahojiano na Redio ya Umoja wa Mataifa, Bwana Jazairy ameeleza kwamba makubaliano kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran hayakufikiwa kwa sababu ya vizuizi tu.

Ameeleza kwamba mara nyingi vizuizi vinasababisha matokeo mabaya kwenye jamii za nchi zinazolengwa na vizuizi hivyo, akichukua mfano wa Iran ambapo watu 85,000 walioathiriwa na saratani wameshindwa kupata matibabu.

Kuelelekea Baraza la Haki za Binadamu mwezi Septemba mwaka huu, mtalaam huyo amesema ni muhimu kupendelea zaidi vizuizi vinavyoamuliwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuliko vizuizi vinavyoamuliwa na nchi moja kwa moja, ili kuimarisha utekelezaji wa vizuizi hivyo, kusikoathiri raia wa nchi zinazolengwa na kuhakikisha sheria ya kimataifa ya kibinadamu inaheshimiwa.