Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mratibu wa Kibinadamu aiomba Israel kuachana na mpango wa kubomoa nyumba Palestina

Mratibu wa Kibinadamu aiomba Israel kuachana na mpango wa kubomoa nyumba Palestina

Mratibu wa maswala ya kibinadamu kwa maeneo yaliyotawaliwa ya Palestina, Robert Piper ameziomba mamlaka za serikali za Israel kusitisha mpango wao wa kubomoa nyumba za wakazi wa eneo la Susiya, lililoko kwenye ukingo wa magharibi wa Palestina.

Taarifa hiyo inafuata ziara yake kwenye eneo hilo pamoja na wawakilishi wa Norway, Uswisi na Italy, ambapo Bwana Piper amesema amekuja kujifunza zaidi kuhusu wasiwasi na hofu za jamii ya eneo hilo.

Nyumba na majengo ya umma ziko hatarini kubomolewa kwenye eneo hilo la Susiya, huku familia kadhaa zikiwa zimeshafukuzwa mara tatu tangu 1986. Sasa hivi Mahakama kuu ya Israel inaangazia mashtaka ya jamii hiyo dhidi ya uamuzi wa kubomoa nyumba zao.

Bwana Piper amesema kubomoa nyumba binafsi ni ukiukaji wa haki ya kimataifa ya kibinadamu, akisema jamii ya kimataifa haitaweza kunyamaza mbele ya vitendo hivyo.