Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Januari hadi Juni 2015 kipindi chenye joto jingi zaidi katika historia- WMO

Januari hadi Juni 2015 kipindi chenye joto jingi zaidi katika historia- WMO

Kipindi cha kati ya Januari na Juni mwaka 2015 kimeingia katika rekodi kama chenye joto jingi zaidi duniani katika historia ya uwekaji kumbukumbu za viwango vya joto, kwa mujibu wa ripoti iliotolewa leo na mamlaka ya kitaifa ya bahari na anga Marekani, na ambayo imechapishwa kwenye tovuti ya Shirika la kimataifa la hali ya hewa, WMO.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kiwango wastani cha nyuzi joto kilizidi kile cha karne iliyopita cha nyuzi 15.5°C (59.9°F),  kwa nyuzi 0.85°C (1.53°F), na pia kuzidi rekodi iliyowekwa awali ya mwaka 2010 kwa nyuzi 0.09°C (0.16°F).

Kiwango wastani cha joto juu ya bahari duniani kilikuwa nyuzi +0.65°C (+1.17°F) na hivyo kuweka rekodi mpya, huku kile cha joto kwenye ardhi kikiwa +1.40°C (2.52°F) ambayo pia ni rekodi mpya, ikizidi ya zamani ya mwaka 2007 kwa nyuzi 0.13°C (0.23°F). Maeneo mengi ya ardhi duniani yalikuwa na joto jingi zaidi kuliko viwango vya kawaida, yakiwemo Eurasia, Amerika ya Kusini, Afrika, magharibi wa Amerika ya Kaskazini, na Australia nzima.