Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uimarishaji wa polisi nchini Somalia unahitajika ili kuimarisha usalama

Uimarishaji wa polisi nchini Somalia unahitajika ili kuimarisha usalama

Ni muhimu kuimarisha taasisi za kiusalama na kuwezesha jeshi la kitaifa la Somalia aidha sekta zima ya usalama na hatimaye kukabidhi majukumu yote ya kiusalama kwa wasomali. Huo ni ujumbe wa Naibu Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwenye operesheni za ulinzi wa amani Edmund Mulet kwa Baraza la Usalama.

Bwana Mulet akihutubia kikao hicho kuhusu Somalia amesema kwamba licha ya hatua zilizopigwa na ujumbe wa Muungano wa Afrika nchini Somalia AMISOM dhidi ya Al Shabab ama bado ni tishio katika ukanda huo ikiwemo nchini Kenya.

Kwa mantiki hiyo Mulet amesema kwamba kukamilishwa kwa makubaliano mapya kuhusu mpango wa polisi ni muhimu na usaidizi wa muda mfupi unahitajika vilevile kuongezwa kwa polisi wa AMISOM ambao watasaidia katika utekelezaji na kutoa mafunzo.

Kwa upande wake  mwakilishi wa Somalia kwenye Umoja wa Mataifa Awale Ali Kullane amesema kwamba hatua zimepigwa akitolea mfano kwamba Al Shabab kwa sasa haitawali maeneo mengi nchini Somalia lakini bado wana uwezo wa kushambulia jeshi la kitaifa na AMISOM.

(SAUTI AWALE)

Tunasikitishwa na uharibifu mkubwa uliotekelezwa katika kipindi cha Ramdan. Ijumaa iliyopita, Al Shabaab wamefanya mashambulizi Mogadishu. Kwa mara nyingine mashambulizi hayo yalilaaniwa , lakini tunapaswa  kusambaratisha uwezo wa Al Shabab wa kutekeleza mashambulizi hayo.”

Ameongeza kwamba lengo kuu la Somalia ni kuona kwamba usalama wa wa nchi uko mikononi mwa jeshi la kitaifa na hiyo kutolea wito jamii ya kimataifa kusaidia katika kutekeleza hilo.