Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM utaunga mkono uteuzi wa Museveni kusuluhisha Burundi:

UM utaunga mkono uteuzi wa Museveni kusuluhisha Burundi:

Umoja wa Mataifa umesema una taarifa ya makubaliano yaliyofikiwa wakati wa kikao cha siku moja cha wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC kuhusu Burundi na kwamba unakaribisha kuchaguliwa kwa Rais Yoweri Museveni wa Uganda kama msuluhishi kati ya serikali na upinzani kwenye mzozo unaoendelea nchini humo.Hiyo ni kauli ya msemaji wa Umoja huo Stephane Dujarric alipokuwa akijibu swali wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini New York, Marekani ambapo aliulizwa chombo hicho kinapokeaje uamuzi wa jumuiya hiyo ya kuteua msuluhishi mpya na pendekezo la kusogeza mbele uchaguzi wa Rais nchini Burundi uliopangwa kufanyika tarehe 15 mwezi huu.

(Sauti ya Dujarric)

“Bila shaka tutaangalia vile ambavyo Rais Museveni ananuia kusongesha mbele muundo huu wa sasa, lakini kile muhimu ni kwamba Umoja wa Mataifa utaunga mkono jitihada hizi ili ziwezes kusaidia kuweka mazingira bora kwa uchaguzi nchini Burundi.”

Bwana Dujarric amesema si suala la mjadala kuwa hali ya Burundi ni changamoto kubwa lakini ni matumaini ya Umoja wa Mataifa kuwa Rais Museveni atatumia muundo huo mpya wa usuluhishi.