Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UN Global Compact imechanua kuliko ilivyotarajiwa: Ban

UN Global Compact imechanua kuliko ilivyotarajiwa: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema miaka 15 ya UN-Global Compact imeleta mabadiliko makubwa katika ushirikiano kati ya Umoja wa Mataifa na wadau wake ikiwemo wafanyabiashara, wasomi n ahata wanamazingira.

Akizungumza katika maadhimisho hayo mjini New York,Marekani, Ban amesema chombo hicho ambacho ni jukwaa la kubuni, kutekeleza, na kuweka wazi sera endelevu za ufanyaji biashara lilianza kama wito tu wa kawaida lakini sasa limekuwa kichocheo cha kubadilisha maisha ulimwenguni.

Amesema kwa sasa Global Compact ina wadau wa biashara zaidi ya 8,000 walioazimia kufanya biashara wajibikaji kwa misingi inayozingatia haki za binadamu, haki za ajira, ulinzi wa mazingira na kuondokana na rushwa.

Ban amesema kuelekea upitishaji wa malengo ya maendeleo endelevu mwezi Septemba mwaka huu, UN Global Compact itakuwa na nafasi kubwa zaidi katika kufanikisha malengo hayo  kwa kuwa..

(Sauti ya Ban)

“Maendeleo endelevu siyo hisani. Ni uwekezaji maridadi. Malengo ya maendeleo endelevu yanatoa fursa ya kipekee kwa uwekezaji na jukwaa la sekta ya biashara kuchanua. Tunavyoingia katika zama mpya, Global Compact itaendelea kutupatia fursa mbali mbali za kuimarisha jitihada hizo ili kufikia mafanikio makubwa.”

 Jukwaa hilo la Global Compact linafikia nchi masikini na tajiri likijumuisha nchi 170.