Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO yatoa wito mifumo ya afya Nepal ikarabatiwe haraka

WHO yatoa wito mifumo ya afya Nepal ikarabatiwe haraka

Shirika la Afya Duniani, WHO, limetoa wito mifumo ya afya nchini Nepal ikarabatiwe haraka ili kuepusha hatari inayowakabili manusura wa tetemeko la ardhi, ambao hawawezi kupata huduma za afya.

WHO imesema wadau wote wanapaswa kushirikiana na kufanya kazi ya kukwamua mapema na kuikarabati miundo mbinu ya afya ya nchi hiyo.

Akizungumza mjini Kathmandu wakati wa kongamano la kimataifa kuhusu ukarabati wa Nepal, Dkt. Poonam Khetrapal, ambaye ni Mkurugenzi wa WHO kwa ukanda wa Kusini Mashariki mwa Asia, amesema kuwa kuna haja ya dharura ya kurejesha huduma za afya kwa mamilioni ya watu walioathiriwa, hususan waja wazito, watoto wachanga, watoto, wazee, watu wenye magonjwa kama kifua kikuu, maradhi ya moyo na kisukari.

Baada ya kupoteza makazi yao kufuatia tetemeko la ardhi nchini mwao mnamo mwezi Aprili mwaka huu, raia wa Nepal waliolazimika kuhama wanaishi katika makazi ya muda, katika mazingira yasiyotimu kiwango wastani cha upatikanaji huduma za kujisafi na maji safi.