Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kudhibiti rushwa na kodi ni mwarubaini wa kuzuia utoroshwaji haramu wa fedha Afrika: Hamdok

Kudhibiti rushwa na kodi ni mwarubaini wa kuzuia utoroshwaji haramu wa fedha Afrika: Hamdok

Kupambana na rushwa na udhibiti wa kodi ni moja ya mapendekezo katika kudhibiti utoroshwaji wa fedha kutoka bara la Afrika amesema naibu katibu mtendaji wa kamisheni ya uchumi kwa ajili ya Afrika ECA,  Abdallah Hamdok.

Katika mahojiano maalum na Derrick Mbatha wa  idhaa ya Kingereza ya redio Umoja wa Mataifa Bwana Hamdok amesema kuwa tatizo la utoroshwaji haramu wa fedha kutoka bara la Afrika ni kubwa mbapo kiasi cha dola bilioni 50 huondoshwa barani humo kila mwaka huku akisema kuwa kiasi hicho chaweza kuwa mara mbili.

Hata hivyo amesema fedha hizo zaweza kurejeshwa barani Afrika kwani jopo maalum linaloongozwa na Rais mstaafu wa Afrika Kusini Thabo Mbeki  limefanya mashauriano na wadau mbalimbali ikiwamo nchi za Ulaya. Amesema mbali na kudhibiti mifumo ya kodi na rushwa mapendekezo mengine ni

(SAUTI HAMDOK)

"Kushugulikia masuala ya utawala wa kibenki,pia kuna suala la biashara na uhalifu, kuimarisha uwezo wa nchi na ushirikiano na pande nyingine. "

Amesema kupitia mkutano wa uchangiaji wa fedha kwa ajili ya maendeleo mwezi Julai nchini Ethiopia utajadili suala hili kwa kina hatua inayofufua matumaini kwa bara hilo.