Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wasichana washika usukani Twitter ya UNICEF kutokomeza ndoa za utotoni

Wasichana washika usukani Twitter ya UNICEF kutokomeza ndoa za utotoni

Katika hatua ya kipekee, wasichana watano kutoka Afrika leo wanatumia akaunti ya Twitter ya shirika la kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF kuelezea madhila waliyopitia kwa kuozwa utotoni na kile ambacho kinapaswa kufanyika ili kuokoa kizazi cha sasa. Taarifa zaidi na Priscilla Lecomte.

(Taarifa ya Priscilla)

Wasichana hao wenye umri wa kati ya miaka 22 hadi 30 hivi sasa ni kutoka Chad, Sierra Leone, Somalia na Uganda wanatuma ujumbe huo kupitia akaunti hiyo yenye wafuasi zaidi ya Milioni Nne ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya mtoto wa Afrika.

Miongoni ni Jennifer kutoka Uganda ambaye anasema alitekwa akiwa na umri wa miaka 13 na kuozwa kinguvu akiwa na umri wa miaka 14 huko Sudan kwa kamanda wa waasi wa Lord’s Resistance Army.

Amesema simulizi yake ni fursa pekee kuchangia kampeni ya kutokomeza ndoa za utotoni barani Afrika.

Takwimu zinaonyesha kuwa duniani kote zaidi ya wanawake Milioni 700 walioko hai hivi sasa waliozwa utotoni na wengi wao wako nchi za Afrika kusini mwa jangwa la Sahara.