Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Maelfu ya wanawake na watoto wakimbia Sudan Kusini

Maelfu ya wanawake na watoto wakimbia Sudan Kusini

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR limesema raia 14,000 wa Sudan Kusini wengi wao wanawake na watoto wamekimbilia Sudan mwishoni mwa wiki.

Kwa mujibu wa shirika hilo hali hiyo imeibua udharura huko wanakokimbilia ambapo hadi sasa raia wa Sudan Kusini waliosajiliwa nchini humo ni 160,000 tangu kuzuka kwa mzozo nchini mwao Disemba 2013.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric akinukuu UNHCR amesema kipaumbele cha sasa cha jamii ya kimataifa ni kujiandaa kwa usaidizi wakati huu ambapo msimu wa mvua unatarajiwa kuanza wiki ijayo na hivyo kukwamisha usambazaji wa misaada.

(Sauti ya Dujarric)

“Kuchua hatua za haraka kuhakikisha upatikanaji wa maji, huduma za kujisafi na usafi ni muhimu kwa kuwa mvua zinaweka mazingira ya magonjwa yanayoenezwa kwa njia ya maji kama vile kuhara na kipindupindu. Hadi sasa ombi la usaidizi wa wakimbizi wa Sudan Kusini la dola Milioni 152 limefadhiliwa kwa asilimia 10 tu.”

Wakati huo huo, hali ya kibinadamu huko Sudan Kusini kwenyewe imezidi kudorora katika kipindi cha miezi miwili iliyopita kutokana na kushika kasi kwa operesheni za kijeshi kwenye majimbo ya Unity na Upper Nile.