Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watu Milioni 400 bado hawapati huduma za afya

Watu Milioni 400 bado hawapati huduma za afya

Ripoti mpya ya Shirika la Afya duniani WHO na Benki ya Dunia inaonyesha kwamba watu milioni 400 duniani kote bado hawapati huduma za msingi za afya, na asilimia Sita ya watu kwenye nchi zenye kipato cha chini au cha wastan wanasukumwa kwenye umasikini kwa sababu ya matumizi ya fedha nyingi zaidi kwenye afya.

Ripoti hii ya pamoja iliyotolewa leo imeangalia upatikanaji wa huduma zote za afya zikiwemo mpango wa uzazi, huduma za wanawake wajawazito, chanjo kwa watoto, dawa za kupunguza makali ya ukimwi, ARV, dawa za kutibu kifua kikuu na upatikanaji wa mafi safi na kujisafi kwa mwaka 2013.

Akihojiwa na redio ya Umoja wa Mataifa, Tessa Tan Torres Edejer, Mratibu wa Maswala ya mifumo ya afya wa WHO, ameeleza kwamba sababu ya kwanza ya kukosa huduma za msingi ni umaskini.

“ Hawapati huduma hizo kwa sababu hawana pesa ya kutosha kwa matibabu watakayopaswa kulipa, mfano dawa au chanjo. Pia inawezekana kwamba wanaishi mbali na vituo vya afya, na hawana pesa ya kwenda kituo cha afya. Sababu nyingine pia ni kwamba, hata kama vituo vya afya vipo, huenda havina dawa au wafanyakazi kuwahudumia.”

Marie-Paule Kieny, Msaidizi wa Mkurugenzi Mkuu wa WHO, amesema serikali zinapaswa kuwapatia huduma za afya watu maskini zaidi, wanawake na watoto, wale wanaoishi mbali na wale kutoka vikundi vya walio wachache.

WHO na Benki ya Dunia zinapendekeza kuwa serikali zinazotaka kutekeleza huduma za afya kwa wote zilenge angalau asilimia 80 ya watu huku hata hivyo yakifurahia kuweza kupima mafanikio katika swala hilo kwa mara ya kwanza, yakisema ripoti zingine kama hii zitatolewa kila mwaka, ili kutathmini mafanikio ya nchi katika kufikisha huduma za afya kwa wote