Athari za muda mrefu za ajira za utotoni zabainishwa na ILO
Ikiwa leo ni Siku ya Kupinga Ajira za Utotoni Duniani, ripoti mpya ya Shirika la Ajira Duniani, ILO inasema kuwa takriban asilimia 20 hadi 30 ya watoto katika nchi za kipato cha chini huacha shule na kuingia katika soko la ajira wanapotimu umri wa miaka 15.
Ripoti hiyo pia inasema kuwa wengi wa watoto hao huajiriwa utotoni hata kabla ya kutimu umri huo.
Ripoti hiyo yenye kichwa: Kufungua njia za ajira zenye hadhi kwa vijana, imebainisha kuwa kwa kawaida, vijana waliobeba mzigo wa ajira wakiwa watoto, hujikuta wanafanya ajira bila malipo nyumbani au kutumbukia ajira za malipo ya chini.
Mkurugenzi Mkuu wa ILO, Guy Ryder, amesema ripoti hiyo inadhihirisha haja ya kuwa na sera yakinifu za kukabiliana na ajira za utotoni na ukosefu wa ajira zenye hadhi kwa vijana.
Amesema kuwapa watoto elimu nzuri hadi pale wanapotimu umri unaofaa kwa ajira, kunaamua ni aina gani ya maisha watoto hao wataishi.