Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wakandarasi waliotekwa nyara Januari huko Darfur waachiliwa huru

Wakandarasi waliotekwa nyara Januari huko Darfur waachiliwa huru

Hatimaye wakandarasi wawili wa ujumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Muungano wa Afrika huko Darfur, UNAMID ambao walitekwa nyara tarehe 29 mwezi Januari mwaka huu wameachiliwa huru.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa amemnukuu Katibu Mkuu Ban Ki-moon akishukuru kwa dhati hatua hiyo iliyotokana na jitihada za UNAMID sanjari na serikali za Sudan na Urusi ambazo ziliwezesha kuachiliwa huru salama kwa wakandarasi hao.

Ban amesema anatiwa moyo kuwa wakandarasi hao waliotekwa nyara huko Zalingei, Darfur Kati, sasa wanaweza kuungana na familia zao baada ya siku 128 za kushikiliwa.

Katibu Mkuu amesisitiza umuhimu wa kazi ya UNAMID kwa mustakhbali wa wakazi wa Darfur na kutoa wito kwa serikali ya Sudan kuchunguza kwa kina tukio hilo.