Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bado watu karibu milioni 3 wahitaji msaada Nepal

Bado watu karibu milioni 3 wahitaji msaada Nepal

Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu OCHA imesema kwamba bado watu milioni 2.8 wanahitaji misaada ya kibinadamu nchini Nepal baada ya matetemeko ya ardhi yaliyokumba nchi hiyo mwezi Aprili na Mei mwaka huu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na OCHA, ni dola milioni 120 tu ambazo zimefadhiliwa hadi sasa, wakati maombi ya fedha yaliyotolewa ni dola milioni 422.

Mpaka sasa hivi, mashirika ya kibinadamu yanaweka kipaumbele katika kutengeneza makazi ya muda kwa ajili ya watu ambao nyumba zao zimeharibika kabisa au kwa kiasi fulani.

Jamie Mc Goldrick, mratibu wa misaada ya kibinadamu nchini Nepal, amesema cha msingi ni kufikisha misaada kwenye maeneo yaliyo mbali zaidi, wakati huu ambapo msimu wa mvua unakaribia.