Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afrika yaonyesha maendeleo katika kupunguza wenye njaa kwa nusu

Afrika yaonyesha maendeleo katika kupunguza wenye njaa kwa nusu

Bara Afrika limepiga hatua katika kupunguza idadi ya watu wenye lishe duni na njaa kwa nusu ifikapo mwaka 2015, huku nchi saba za Afrika zikiwa tayari zimetimiza malengo hayo ya milenia na Mkutano wa Dunia kuhusu Chakula. Taarifa kamili na Amina Hassan ...

(Taarifa ya Amina)

Kulingana na toleo la kwanza la tathmini ya kikanda kuhusu kutokuwa na uhakika wa chakula barani Afrika mwaka 2015, Angola, Djibouti, Cameroon, Gabon, Ghana, Mali na Sao Tome na Principe zimetimiza lengo la milenia la kupunguza kwa nusu idadi ya wenye lishe duni na lile la Mkutano wa Dunia kuhusu Chakula la kupunguza kwa nusu idadi ya wenye njaa.

Afrika Magharibi hasa imeonyesha kupiga hatua kwa kupunguza kuenea kwa lishe duni kwa asilimia 60 katika ripoti ya tathmini hiyo ya Shirika la Chakula na Kilimo, FAO.

Akizungumza kuhusu ripoti hiyo, Bukar Tijani ambaye ni Msaidizi wa Mkurugenzi Mkuu wa FAO na Mwakilishi wake kwa ukanda wa Afrika, amesema kuwa idadi ya wenye njaa imepungua kwa milioni 11 ukanda wa Afrika Magharibi, licha ya kuongezeka idadi ya watu kwa kasi na ukame wa mara kwa mara katika nchi za Sahel.