Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mlinda amani mmoja wa Umoja wa Mataifa auawa Mali

Mlinda amani mmoja wa Umoja wa Mataifa auawa Mali

Walinda amani wawili waliokuwa wanasafiri kwenye gari la Umoja wa Mataifa nchini Mali wameshambuliwa na kupigwa risasi kwenye maeneo ya uwanja wa ndege wa Bamako, jumatatu usiku ambapo mmoja wao amefariki dunia kutoka na majeraha.

Hii ni kwa mujibu wa msemaji wa Umoja wa Mataifa, Stephane Dujarric, alipozungumza na waandishi wa habari leo mjini New York.

Bwana Dujarric amesema Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Mali MINUSMA na serikali ya Mali tayari wanachunguza ili kuelewa ni nini kilichotokea na kwamba hadi sasa hakuna taarifa zaidi.

Shambulio hilo limetokea wakati ambapo mapigano yanazidi kuongezeka kaskazini mwa nchi hiyo na kulazimika maelfu ya raia kukimbia makazi yao.