Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban awa na mazungumzo na marais wa Ukraine na Poland:

Ban awa na mazungumzo na marais wa Ukraine na Poland:

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon aliyeko ziarani Ulaya, amekuwa na mazungumzo ya utatu na Rais wa Poland Bronislaw Komorowski na yule wa Ukraine Petro Poroshenko.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa amesema mazungumzo hayo yanafutia ombi la Rais Komorowski ambapo viongozi hao watatu wamebadilisha mawazo kuhusu mzozo unaoendelea nchini Ukraine ambapo Katibu Mkuu ametumia fursa hiyo kusihi pande zote kutekeleza hima na kikamilifu makubaliano ya Minsk.

Bwana Ban, kwa kina ametambua umuhimu wa kuwepo kwa sitisho la mapigano la kudumu na kujaribu kusongesha vifungu vya kisiasa ndani ya makubaliano hayo.

Katibu Mkuu ametumia fursa hiyo kuwashukuru marais hao kwa mwaliko wao kwake wa kuhudhuria sherehe za kumbukizi  ya kumalizika kwa vita kuu ya pili ya dunia zinazofanyika leo huko Gdansk Poland na kesho huko Kiev.