Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WFP yaendelea kusambaza msaada wa chakula nchini Nepal

WFP yaendelea kusambaza msaada wa chakula nchini Nepal

Ndege ya shirika la mpango wa chakula duniani WFP iliyokuwa imesheheni msaada wa chakula, tani 50 za biskuti za kuongeza nguvu imewasili mjini Kathmandu kwa ajili ya kusambaza haraka chakula hicho kwa maelfu ya watu walioathirika na tetemeko la wiki iliyopita.

WFP jana Jumatano ilianza ugawaji wa chakula katika wilaya za Gorkha na Dhading na leo na siku zijazo inaendelea na ugawaji katika wilaya zingine zilizoathirika Zaidi.

Katika huduma zake za dharura WFP pia inasaidia masuala ya kiufundi kwa jumuiya nzima ya huduma za kibinadamu na inatumia kituo chake kwenye uwanja wa ndege  mjini Kathmandu kusaidia kuratibu misaada inayoingia kwa ndege za mizigo.

WFP pia imesema inahitaji dola milioni 116.5 ili kuweza kutoa chakula kwa watu milioni 1.4 katika eneo la Kati na Magharibi mwa Nepal kwa muda wa miazi mitatu.