Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Christiane Amanpour wa CNN atangazwa kuwa balozi mwema wa UNESCO

Christiane Amanpour wa CNN atangazwa kuwa balozi mwema wa UNESCO

Mwandishi habari mashuhuri na mkuu wa waandishi habari wa kimataifa kwenye shirika la kimataifa la utangazji la CNN Bi Christiane Amanpour ametangazwa kuwa balozi mwema wa shirika la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO kuhusu uhuru wa kujieleza na usalama wa waandishi habari .

Hafla maalumu ya kumtangaza imefanyika kwenye makao makuu ya UNESCO mjini Paris Ufaransa. Mkurugenzi mkuu wa UNESCOametangaza Bi Amanpour kwa kutambua juhudi zake za kuchagiza vyombo vya habari huru, visivyoingliwa na vya tabaka na tamaduni tofauti.

Mkurugenzi wa UNESCO Bi Irina Bokova amesema katika hali ngumu, kushughulikia mahitaji ya waliowengi, ujasiri na uadilifu daima vimekuwa muongozi wa Christiane Amanpour.

Katika hotuba yake ya kukubali jukumu hilo Bi amanpour amesisitiza umuhimu wa jukumu la waandishi wa habari kama nguzo ya mabadiliko, uhuru na demokrasia ambayo kazi yake ni kuimarisha jumuiya za kijamii. Amesema waandishi habari wako hapa kujenga dunia kuwa mahala bora.

Pia ametoa ombi maalumu la kuachiliwa wanahabari wote walioko jela, popote walipo, na kulaani ongezeko la mashambulizi na mauaji ya wanahabari. Kutangazwa kwa Bi Amanpour kumefanyika siku chache kabla ya siku ya kimataifa ya uhuru wa vyombo vya habari duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka Mai 3.