OCHA yaonya kuhusu hali ya kibinadamu Yemen
Tangu mwanzo wa mapigano ya angani yaliyoanza nchini Yemen tarehe 26 Machi, ni zaidi ya watu 120,000 ambao wamelazimika kuhama makwao, hasa kwenye maeneo ya kaskazini mashariki mwa nchi.
Hii ni kwa mujibu wa Jens Laerke, msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu, OCHA, akizungumza leo na waandishi wa habari mjini Geneva. Amesema kwamba mashirika ya kibinadamu yanajitahidi kutoa msaada wa huduma za maji, afya na kuondoa maji taka, lakini ukosefu wa usalama unakwamisha ufikishaji wa msaada huo.
Ameongeza kwamba ni vigumu kuthibitisha takwimu hizo kwa sababu watu wanazidi kukimbia.
Aidha Mkuu wa OCHA nchini humo ameomba pande zote zisitishe mapigano kwa muda ili kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Yemen na kusambazwa.
Ameongeza kuwa wadau wa kibinadamu wanatarajia kutoa wito kwa wafadhili ili kutimiza mahitaji ya maelfu ya watu katika mzozo huu wa Yemen.